Geita, Mei 2025
Mkuu wa Mkoa wa Geita, Mhe. Martine Shigela, amepiga marufuku vitendo vya kuwarudisha wanafunzi nyumbani kwa sababu ya michango inayokubaliwa na wazazi katika ngazi ya kijiji au kitongoji, akisisitiza kuwa haki ya mtoto kupata elimu ni ya msingi na haihusishwi na michango.
Akizungumza katika ziara ya siku moja aliyoifanya kwenye kata za Nyamigota na Nyamwilolelwa, Mhe. Shigela amesema kuwa uamuzi wowote kuhusu michango unapaswa kutekelezwa kwa kushirikisha wazazi bila kuathiri masomo ya watoto.
Katika kata ya Nyakagomba, Mkuu huyo wa Mkoa alitembelea bwalo la chakula la Shule ya Sekondari Butundwe, ambalo limekamilika na kuanza kutumika, likigharimu zaidi ya shilingi milioni 366 kupitia mpango wa Uwajibikaji wa Makampuni kwa Jamii (CSR) kwa mwaka 2021/2022. Mhandisi wa Halmashauri, Bi. Beatrice Mwaitete, alisema bwalo hilo litasaidia wanafunzi kupata mazingira salama ya kula chakula na kuokoa muda wa masomo.
Aidha, Mhe. Shigela alifanya mikutano ya hadhara katika kijiji cha CCM (kata ya Nyakagomba) na Saragulwa (kata ya Nyamwilolelwa), ambapo alikagua pia ujenzi wa ofisi ya kata ya Nyamwilolelwa unaogharimu zaidi ya shilingi milioni 94 kupitia mapato ya ndani ya Halmashauri.
Akizungumza kuhusu maendeleo, Mhe. Shigela alisifu kata ya Nyakagomba kwa jitihada za upandaji miti na maendeleo ya mtu mmoja mmoja, akisema, “Nimejionea maendeleo ya kweli kwa watu binafsi; nyumba nzuri na miti iliyopandwa ni viashiria vya maendeleo.”
Kwa upande wake, Diwani wa kata ya Nyamigota na Makamu Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Geita, Mhe. Khadija Saidi, aliipongeza serikali kwa dhamira yake ya kukamilisha miradi ya maendeleo kwa kushirikiana na ofisi ya Mkuu wa Wilaya.
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri, Ndg. Karia Magaro, alisema miradi yenye thamani ya zaidi ya shilingi bilioni 59 imetekelezwa ndani ya miaka minne ya uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, ikihusisha sekta za afya, elimu na miundombinu.
Naye Kamanda wa Polisi Mkoa wa Geita, Kamishna Msaidizi Mwandamizi Sophia Jongo, alisema matukio ya wizi wa mifugo yamepungua baada ya kuanzishwa kwa ulinzi shirikishi. Aidha, alikemea vikali vitendo vya ushirikina, hasa kwa waganga wa kienyeji wanaopiga ramli chonganishi na kutumia viungo vya binadamu, akionya kuwa vitendo hivyo ni kinyume cha sheria.
Katika ziara hiyo, Mkuu wa Mkoa pia alisikiliza na kutoa majibu kwa changamoto mbalimbali zikiwemo maji, miundombinu na ongezeko la mbwa wa mitaani wanaohatarisha usalama wa wananchi.
Halmashauri ya Wilaya ya Geita
Anuani ya Posta: S.L.P 139 Geita
Simu: +225 282520061
Mobile:
Barua pepe: info@geitadc.go.tz
Hakimiliki@ Halmashauri ya wilaya ya Geita , Haki zote zimehifadhiwa